MBARONI KWA KUJIPATIA MILIONI 2.1 KWA JINA LA LUKUVI
Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mtu mmoja ambaye ni mkazi wa Mabibo Jijini Dar es salaam (jina linahifadhiwa) akitumia jina la Waziri wa zamani, William Lukuvi kuendesha mafunzo ya ujasiriamali mkoani Kilimanjaro na kujipatia Sh2.1 milioni kupitia mafunzo hayo.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Simon Maigwa amethibitisha kukamatwa kwa mtu huyo, akisema alikuwa akijipatia Sh35,000 kwa kila mshiriki wa mafunzo hayo huku akiwaahidi kuwalipia kila mmoja Sh300,000 kama ada baada ya kuhitimu mafunzo hayo na kwamba atawapatia ajira.
Kamanda Maigwa amesema baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema wakati akiendesha mafunzo hayo katika ukumbi wa polisi Moshi, Jeshi la Polisi lilitumia mbinu za kumnasa mtu huyo.
"Baada ya kupata taarifa hizi jeshi la polisi tuliwasiliana na viongozi ambao mtuhumiwa huyu alikuwa akiwataja ambapo walimkana na kwamba hawamjui, hivyo tunaendelea kumshikilia kwa hatua zaidi," amesema Kamanda Maigwa.
Mtuhumiwa huyo amekuwa akiendesha mafunzo hayo ya ujasiriamali katika mikoa mbalimbali ya Dar es salaam, Tanga, Morogoro, Arusha, Mbeya na Tanga kwa kujipatia kipato isivyo halali.

Maoni